CRDB WANGING'OMBE YAPONGEZWA MAGEUZI YA HUDUMA KWA WATEJA.
Tarehe iliyowekwa: October 12th, 2025
Na. Nickson Kombe,
BENKI ya CRDB, Tawi la Wanging'ombe yapongezwa na wateja wake wa Halmashauri ya wilaya ya Wanging'ombe kutokana na mageuzi ya Teknolojia ya Habari na mawasiliano (TEHAMA) katika utoaji wa huduma zake na kupelekea huduma bora kwa wateja wao.
Akizungumza na menejimenti ya Halmashauri ya wilaya ya Wanging'ombe, Meneja biashara wa Kanda ya Nyanda za juu kusini, Bi. Domina Mwita amesema kutokana na mageuzi makubwa ya Teknolojia ya Habari na mawasiliano (TEHAMA) wanaendelea na sera ya kuhudumia wateja bila kufika ofisini au kwenye matawi ili kumpunguzia mteja gharama na muda.
Hata hivyo Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Wanging'ombe, Dkt. Peter Maiga Nyanja amewapongeza kwa huduma bora ambazo wameendelea kuzitoa kwa watumishi na wananchi wilayani humo. Haswa ukizingatia kampeni yao ya "Ulipo tupo" imefanikiwa kufikisha huduma za kifedha vijijini na kuhudumia watanzania wote.
Aidha Benki ya CRDB, Tawi la Wanging'ombe imehitimisha wiki ya huduma kwa wateja 2025 yenye kauli mbiu: "Mission Possible" kwa kudumisha mahusiano mazuri na wateja wake wa halmashauri ambapo wamejumuika kupata kifungua kinywa kizito na menejimenti hiyo.