ZIARA YA MBUNGE, MWAKILISHI WAFANYAKAZI TANZANIA, WANGING’OMBE
Tarehe iliyowekwa: November 17th, 2023
Na. Mwandishi Wetu,
Nickson Kombe,
MBUNGE Viti maalumu anayewakilisha Wafanyakazi Tanzania, Mhe. Dkt. Alice Kaijage ametembelea Halmashauri ya Wilaya ya Wanging’ombe mkoani Njombe ambapo ameongea na watumishi kuhusu namna bora ya kushughulikia changamoto zao.
Akiongea na Watumishi baadhi waliohudhuria kikao hiko, Ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Wanging’ombe, Mhe. Dkt. Alice amewapongeza kwa kazi kubwa wanazofanya bila kujali changamoto wanazo kabiliana nazo katika utendaji kazi.
Mara baada ya kuwasikiliza watumishi hao, kwa utaratibu wa kuchangia na uandishi, maoni, ushauri, pongezi na changamoto mbalimbali wanazopitia kazini, Mhe. Dkt. Alice ameomba kupata ufafanuzi wa baadhi ya changamoto kutoka kwa viongozi waliokuwepo ambapo amesema baadhi ataziwasilisha serikalini ili kufanyiwa marekebisho na kutolewa maamuzi. Hivyo watumishi wa umma waendelee kufanya kazi katika mazingira rafiki.
Aidha bajeti zote kuanzia ya Mwaka wa fedha 2021/22 hadi hivi sasa, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanya jitihada za dhati ambapo imeweza kupandisha madaraja /vyeo takribani watumishi 455,497 ikiwa imegharimu zaidi ya Shillingi Trillioni 1.1. Malipo ya malimbikizo ya mishahara ya watumishi wapatao 130,166. Aidha ajira mpya kwa watanzania 129,084 na utekelezaji wa mpango wa ajira 47,000, ajira za TAMISEMI zaidi ya nafasi 21,000 katika Mwaka huu wa fedha 2023/24.
Katika Ziara hiyo Mkoa wa Njombe, Mhe. Dkt. Alice ameambatana na Mwakilishi Ofisi ya RAS Njombe, Mratibu wa TUCTA na Wawakilishi wa Vyama vya wafanyakazi vya CWT, TALGHU, TUGHE na TIPAU.
“Nasema haya ikiwa sisi sote ni shuhuda ya kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imekuwa Sikivu na imeonyesha nia njema ya kuboresha maslahi na haki mbalimbali za watumishi wa umma”. Mhe. Dkt. Alice ametoa rai kuendelea kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kufanya kazi kwa bidii na uadilifu.