MAKAMU WA RAIS, MHE. DKT. PHILIP MPANGO AELEKEZA MAMLAKA ZA ARDHI KUSULUHISHA MGOGORO WA MIPAKA YA WILAYA ZA WANGING'OMBE NA MAKETE
Tarehe iliyowekwa: October 27th, 2023
Na. Nickson Kombe,
Makamu wa Rais, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango ameelekeza usuluhishi wa mipaka ya Wilaya za Wanging'ombe na Makete akiwa kwenye ziara mkoa wa Njombe, Kata ya Kipengere.
Akisikiliza changamoto zinazowakabili wananchi wa Jimbo la Wanging'ombe, Mhe. Mpango ametoa muda usiozidi siku 30, wataalamu kutoka Wizara ya Ardhi na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa zikishirikiana na Halmashauri zote mbili kufanya kikao wakiwa eneo husika katika kijiji cha Moronga kilichopo mpakani ili kuondoa utata wa muda mrefu uliopo na kuacha kusumbua wakulima na wafanyabiashara katika zoezi la ukusanyaji mapato ya Halmashauri hizo.
Hata hivyo baada ya maelekezo hayo, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Anthon Mtaka amesema utekelezaji wa tamko hilo umepokelewa na utafanyiwa kazi na wataalamu pamoja na viongozi wanaohusika watakapokutana kijiji cha Moronga, akinukuliwa kwa msemo wa "Mgogoro wa Shamba usuluhishwa Shambani..." Hivyo timu ya wataalamu kutoka Wizara ya Ardhi, Mkoa na Halmashauri pamoja na viongozi watakutana saiti ili kumaliza changamoto iliyopo.
Akitolea ufafanuzi wa Mgogoro huo, Diwani Kata ya Kipengere, Mhe. Mussa Sanga ameomba mamlaka za ardhi kurahisisha zoezi hilo kwa kuleta nyaraka za uratibu wa jiografia za mwaka 1980 na kuondoa utata uliopo.
Aidha wananchi wa Kata ya Kipengere ambao wamehudhuria mkutano huo wamesema wanakumbana na changamoto za usumbufu wa utozwaji ushuru mara mbili getini pindi wanapo safirisha mazao yao na bidhaa nyinginezo. Na kupelekea kukwepa tozo hivyo kuikosesha mapato serikali.