Na. Baraka Tarimo,
KAMA ilivyo sera ya Utunzaji na Uhifadhi wa Mazingira ya Serikali Awamu ya Sita, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameelekeza kila wilaya kuendelea kupanda na kuitunza miche ya miti ili kuweza kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.
Akiongoza zoezi hilo leo tarehe 11 Februari 2026, Mkuu wa wilaya ya Wanging'ombe, Mhe. Zakaria Saili Mwansasu amehakikisha miche ya miti 2,000 ya aina Mdodoma, Krismasi n.k kupandwa pembezoni wa barabara za mji wa Igwachanya uliopo wilayani Wanging'ombe.
Mhe. Mwansasu ametumia fursa hiyo kuwakumbusha watumishi wa umma na wananchi kuhusu mpango mkakati wa kitaifa wa upandaji miti takribani milioni 1.5 Kila mwaka, ambapo Katika msimu wa mwaka 2025/2026, jumla ya miche 2,244,334 imeoteshwa, sawa na asilimia 149.6 ya lengo.
Mkuu wa Wilaya amewataka viongozi ngazi ya kata, vijiji na vitongoji kuendelea kuhamasisha wananchi kushiriki katika kampeni za upandaji miti na kuhakikisha miti iliyopandwa inalindwa na kutunzwa ipasavyo kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Aidha Halmashauri ikiwakilishwa na Mkuu wa Kitengo cha Maliasili na Uhifadhi wa Mazingira Bw. Kasmir David ametoa shukrani kwa wadau mbalimbali wakiwemo Ofisi ya Makamu wa Rais – Mazingira, TANWAT, One Acre Fund Tanzania na TFS kwa mchango wao katika uoteshaji, upandaji na uhifadhi wa miti.















Copyright ©2021 Wanging'ombedc . All rights reserved.