MAKABIDHIANO MRADI WA UJENZI WA BARABARA KIWANGO CHA LAMI (ITULAHUMBA - IGWACHANYA)
Tarehe iliyowekwa: November 25th, 2023
Na. Mwandishi Wetu,
Nickson Kombe,
Naibu Waziri TAMISEMI, Mbunge wa Wanging'ombe, Mhe. Dkt. Festo Dugange amekabidhi makisio ya Mradi wa Ujenzi wa Barabara Kiwango cha Lami (Itulahumba - Igwachanya) umbali wa Kilomita 19.25 yenye thamani zaidi ya Shilingi Bilioni 9.8 kwa Mkandarasi mzawa Summer Communications Co. Ltd.
Akihotubia Wananchi wa Kata ya Itulahumba na Igwachanya, Mhe. Dkt. Dugange ametoa pongezi za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo ameweza kusikia kilio cha wananchi wa Wanging'ombe ambao wataenda kunufaika moja kwa moja na Ujenzi wa Mradi huo.
Mhe. Dkt. Dugange amesisitiza umuhimu wa Mkandarasi ambae ameshinda zabuni ya Mradi wa Ujenzi wa Barabara hiyo kutoa fursa kwa wazawa/wenyeji ambapo watasaidia katika ulinzi wa malighafi zitakazotumika kufanya ujenzi kwa sababu wao wanafahamu faida watakazonufaika nazo iwapo mradi utakamilika katika ubora unaotakiwa.
Hata hivyo katika hafla hizo za makabidhiano, Mkuu wa Wilaya ya Wanging'ombe, Mhe. Claudia Kitta amesisitiza ugawaji wa fursa katika usawa wa jinsia kitu ambacho moja kwa moja kitaenda kunufaisha familia. Akinukuliwa kwa usemi wa "pesa ya mama inaliwa na familia..."
Katika hafla za makabidhiano hayo zilizofanyika Kata ya Igwachanya na Itulahumba, ambapo makisio ya Barabara hiyo ya kiwango cha lami yameandaliwa na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) itakatiza Kata ya Itulahumba - Kilomita 14.15, Igwachanya - Kilomita 5.10. Aidha Kata zilizopakana na mradi huo kama Imalinyi, Igima, Usuka, Kidugala na Luguda pia zitanufaika kwa urahisi wa usafirishaji wa mazao, maliasili na mifugo.
Wananchi wamefurahishwa na Mradi wa Ujenzi wa Barabara ya Itulahumba - Igwachanya unaotarajiwa kuanza Disemba 05, 2023, ambapo utaenda kupunguza adha ya usafiri wa abiria, mazao, maliasili na mifugo yao haswa kipindi cha mvua.