MAADHIMISHO YA SIKU YA FIMBO NYEUPE KITAIFA – NJOMBE MJINI
Tarehe iliyowekwa: November 28th, 2023
Na. Mwandishi Wetu,
Nickson Kombe,
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Prof. Joyce Ndalichako ameshiriki katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Fimbo Nyeupe Duniani ambapo kitaifa yamefanyika Njombe Mjini, yenye kaulimbiu “Upatikanaji wa Teknolojia fikivu katika Ujenzi wa Uchumi wa Kidijitali ni Mkombozi kwa mtu asiyeona na Taifa”.
Akihotubia washiriki wa vyama vya watu wasiyoona katika kilele cha maadhimisho hayo, Mhe. Prof. Ndalichako amesema Serikali itaendelea kuimarisha Ustawi wa watu wenye ulemavu nchini hususani upande wa elimu, afya miundombinu, ajira pamoja na ushiriki wao katika nafasi mbalimbali kwenye jamii. Ametoa salamu za pongezi kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ametekeleza kaulimbiu ya maadhimisho hayo ikiwa ni pamoja na utoaji wa ajira, ujumuishwaji katika maswala ya TEHAMA, uboreshaji wa miundombinu ya elimu, uwezeshaji kupitia mikopo ya wajasiriamali na upatikanaji wa vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu.
Aidha, Mhe. Prof. Ndalichako ametoa pongezi za dhati kwa wadau wa maendeleo ambapo wameshirikiana na Serikali kutekeleza miradi mbalimbali ya watu wasiyoona hapa nchini ikiwemo WHO, Sightsavers, CBM, My Right, Standing Voice na TLB.
Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Anthony Mtaka amewashukuru wafadhili ambao wamewezesha maadhimisho hayo na kuwaomba washiriki wote kutokusita kurudi mkoani Njombe ili aweze kuwaonyesha mafanikio ya ujasiriamali uliofanywa na watu wasiyoona na kufanikiwa sana.
Makundi ya watu wasiyoona wameshukuru kwa maadhimisho hayo ambapo yameambatana na maandamano ya umbali wa Kilomita 2 kupitia barabara kuu ya Njombe Mjini ikiwa na lengo la kuihamasisha jamii na watumiaji wote wa barabara kama vile madereva, kuiheshimu fimbo nyeupe na kumsaidia asiyeona anapotembea na anapovuka barabara.