MAADHIMISHO SIKU YA WAZEE DUNIANI OKTOBA MOSI - WANGING'OMBE
Tarehe iliyowekwa: October 1st, 2023
Na. Mwandishi Wetu,
Nickson Kombe,
Mkuu wa Wilaya ya Wanging’ombe, Mheshimiwa Claudia Kitta amegawa kadi 89 za msamaha wa matibabu kwa wazee wasio na uwezo ikiwa ni maadhimisho ya sikukuu ya wazee duniani iliyoadhimishwa Oktoba Mosi tarafa ya Mdandu.
Akihutubia Wananchi waliohudhuria Sherehe hizo za Maadhimisho, Mhe. Claudia Kitta amesema wazee ni hazina ya taifa hili hivyo jamii haina budi kuwaheshimu na kuhakikisha wanapata haki zao za kimsingi na kuachana na mila potofu ambazo zimekuwa kandamizi kwa haki za wazee. Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada za dhati za kuleta usawa na ukombozi wa kweli kwa wazee kupitia programu za kuunda mabaraza ya wazee.
Mganga Mkuu wa Wilaya ya Wanging’ombe, Daktari Frank Chiduo amewaasa wazee kuzingatia afya, lishe na matibabu pale ambapo wanapatwa na magonjwa, timu za wataalamu wa afya zinashirikiana kuhakikisha wazee wetu wanakuwa na afya njema.
Mkaguzi Msaidizi wa Polisi, Wilaya ya Wanging’ombe amekemea vitendo vya ukatili katika jamii pia amesema jeshi la polisi na dawati la kijinsia wamejipanga kukabiliana na matukio ya ukatili wa jinsia.
Elimu ya matumizi sahihi ya vyoo vya sato imetolewa na Afisa Afya Wilaya ya Wanging'ombe kwa ajili ya kurahisisha huduma kwa wazee waliodhoofika viungo.
Aidha pamoja na hayo Wazee wa Wilaya ya Wanging'ombe wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa huduma mbalimbali wanazopatiwa ikiwemo Huduma za Afya kwa wazee wasio na uwezo.