Mkuu wa Wilaya ya Wanging'ombe Comrade Ally Kasinge amewahamasisha Wananchi wa Wilaya ya Wanging'ombe kujiunga na mfuko wa Bima ya Afya ya jamii iliyoboreshwa . Mkuu wa Wilaya ameyasema hayo katika kijiji cha Chalowe tarehe 7/11/2019 wakati wa sherehe za uzinduzi wa uandikishaji wananchi katika CHF iliyoboreshwa .
"Nawaagiza wananchi wote kuhakikisha mnajiunga na mfuko wa Bima ya Afya ya jamii iliyoboreshwa kwani ina faida nyingi ikiwemo kutibiwa katika hospital yeyote ya Serikali ndani ya Mkoa na ongezeko la wigo wa huduma za afya tofauti na ilivyokuwa awali " Alisema Kasinge.
Katika uzinduzi huo Mkuu wa Wilaya aliongozana na M/kiti wa Halmashauri, Mkurugenzi Mtendaji na Wataalamu wa afya wa Wilaya pamoja na Afisa TEHAMA Bw Amon Chalamila ambae ndio msimamizi wa mfumo huo. Akitoa hotuba M/kiti wa Halmashauri Mhe Antony Mahwata aliwasisitiza wananchi wajitokeze kwa wingi ili kuweza kutumia fursa hiyo ambayo Serikali ya Awamu ya tano ameamua kuboresha huduma za Afya. Nae Mkurugenzi Mtendaji aliwaasa wananchi kujiunga na CHF iliyoboreshwa ili waweze kupata fursa ya kutibiwa wakati wamepata maradhi.
"Ndugu zangu maradhi huwa hayabishi hodi , unaweza ukapatwa na ugonjwa wakati wowote ule ambapo hauna fedha hivyo kwa kulipia shilingi 30,000/= kwa kaya yenye watu 06 itawasaidia kupata huduma za matibabu muda wowote" Alisema Edes Lukoa.
Mkuu wa Wilaya ametumia fursa hiyo kuwataka wahusika wote kuanzia ngazi ya Wilaya hadi kijiji kuhamasisha wananchi kujiandikisha katika CHF iliyoboreshwa.
Copyright ©2021 Wanging'ombedc . All rights reserved.